Ijumaa, 27 Machi 2015

VIONGOZI WA DINI WANA KIBALI KUINGILIA SIASA

 
Kwa kiasi kikubwa ni bara la Afrika ambapo pana msuguano mkubwa kati ya dini na siasa kuliko bara la Ulaya ambalo ndilo lina kiwango cha juu cha ustaarabu lakini misuguano baina ya viongozi wa dini na wale wa siasa ni nadra sana kutokea. Kijapo kipindi cha uchaguzi ndipo misuguano hii huwa inakolezwa sana kuliko kipindi kingine kiwacho chote kile. Kama kuna sababu kubwa iliyofanya Mungu akaadhibu wafalme na falme zao basi ni kukataa maagizo ya Mungu aliyowafikishia Wafalme kupitia makuhani wake.
Kimsingi nahisi ni suala la kukosa maarifa ya Neno la Mungu kwa upande wa wanasiasa ambao nao wanatoka kwenye nyumba hizi hizi za ibada ambazo zinatumia misaafu kufundishia Neno la Mungu, lakini inaonekana wanasiasa wakiishatoka kwenye nyumba za ibada na wakiishatumia misaafu hii kula kiapo basi wanaachana kabisa na habari ya imani hadi pale wanapohisi wameingia kwenye matatizo ya kisiasa ndipo wanakimbilia tena nyumba za ibada kuomba maombezi ya kuokoa mustakabali wao. Hii ni sanamu!
Biblia iko wazi kabisa jinsi ambavyo Watumishi wa Mungu walikuwa na kibali cha kuingilia kati siasa [political intervention] kwenye falme za nyakati za Biblia na wakafanikiwa sana kuokoa hali ambazo zilikuwa zinaenda ndivyo sivyo na hata kuokoa uongozi wa wafalme hao kama siyo kuokoa ufalme mzima.
Hapa ndipo pana msingi na kibali cha viongozi wa leo wa dini kuingilia siasa na kwamba Neno la Mungu lililowapa Watumishi wake wa nyakati za Biblia kuingilia siasa halijabadilika hata leo, bado ni hilo hilo linalowapa kibali Watumishi wa Mungu/viongozi wa dini wa leo kuingilia kati siasa ili kuokoa mustakabali wa nchi zao.
Ebu tuone ushahidi wa kimaandiko wa Watumishi wa Mungu wa nyakati za Biblia walioingilia siasa ili kuokoa hatma ya watu katika falme hizo: Yusufu aliingizwa kwenye siasa kwa amri ya Farao mwenyewe na kuiokoa Misri Mwa.37:21-36; 39:40; 41:41-45. Danieli aliokoa ufalme wa Dario kutoka utawala wake kufitinika na mfalme akaagiza kuwa watu wote wa ufalme watetemeke mbele za Mungu wa Danieli Dan.6:26. Daniel akafanikiwa sana katika enzi za wafalme Dario na Koreshi Mwajemi Dan.6:28.
Watumishi wa Mungu Nabii Eliya Mtishbi na Gideoni walipindua miungu ya falme kwa kuwachinjilia mbali kondeni manabii 450 na kuthibitisha kuwa Mungu wake ndiye Mungu wa kweli 1Fal.18:21, 22-40; Amu.6:27. Wafalme waliabudu miungu hii ndiyo maana waliruhusu manabii hawa wa uongo kuwepo miongoni mwao kwenye falme zao na huenda waliwapa usajili wa kiserikali kufanya shughuli zao za kinabii zilizoegemezwa kwa miungu ya uongo. Sijajuwa ilimgharimu Nabii Eliya siku ngapi kumaliza kuwaua wale manabii wote 450? Na nachelea kutafakari jinsi ya huo mstuko wa msiba mkuu namna hiyo kuipata dunia.
Mtumishi wa Mungu Yona alisafirishwa tumboni mwa samaki kwa amri ya Mungu bila kufa hadi Ninawi na akafanya huduma yenye upako mkuu Yon.1-4 na kuifanya Ninawi kuweka rekodi duniani na kwa Kanisa; ya mfungo ambao haujawahi kutokea mfano wake isipokuwa ule mfungo wa YESU tu. Mfalme hakuwataka kabisa viongozi wa dini [watumishi wa Mungu], na Yona alipokwenda kwa mara ya kwanza alitishiwa kuuawa au kufungwa jela kwa sababu anakosoa siasa za Mfalme na kuleta mafundisho mageni ambayo siyo ya ufalme lakini mfumo [siasa] wa uendeshaji ufalme ulimkwaza Mungu, ndiyo maana Yona alipoambiwa na Mungu arudi mara ya pili Ninawi akaogopa matishio ya Mfalme na kuamaua kutoroka kwa merikebu.
Lakini kwa kuwa Mungu hakwepeki, Yona hakuwa na namna bali kwenda kuingilia siasa za Ninawi ili iokoke na ghadhabu ya Mungu ya kutaka kukizamisha kisiwa cha Ninawi chini ya bahari kwa kukumbatia uasi kwa Mungu wa kweli. Mfalme alibaini kuwa Yona amepewa kibali kuingilia mfumo wa utawala wa Mfalme na ujumbe wa Mungu kupitia kwa Yona ukamuingia Mfalme na kutoa amri [decree] ya ufalme wote kufunga kwa maombi tena akaenda mbali zaidi kwa kuamuru hata mifugo nayo ifunge, hakuna kula wala kunywa, kisiwa chote kikawa kinanyeshewa tu mvua ya machozi kwa siku tatu mfululizo na ufalme na utawala wa Mfalme vikasalimika.
Yesu Kristo Nabii wa mwisho katika safu ya Manabii wa Mungu wa nyakati za Biblia, alifanya huduma yake kwa kuzishauri falme e.g. wakati anawaambia watu wampe Kaisari yaliyo yake maadamu sura yake iko kwenye sarafu. Ingekuwa ni leo Yesu anaingilia serikali za falme/nchi za nyakati za leo je, wanasiasa wangefanyaje? Je, wangemtundika msalabani? Biblia inasema kazi alizoacha Yesu ndizo hizo wanazofanya Watumishi wa Mungu wa leo na hii inamaanisha kazi ya kuzishauri na kuingilia kati inapobidi; utendaji wa serikali na wanasiasa.
Sasa wale wanaojaribu kuwafunga midomo viongozi wa dini wa leo kutokuingilia siasa hata kama nchi inateketea kwa kigezo kuwa wanaingilia eneo lisilo lao nawaona kama wana tatizo la ombwe kubwa sana la maarifa ya Neno la Mungu na wanastahili msaada wa dharura kuwaokoa ili waendelee kustahili madaraka yao. Tena ni afadhali viongozi wa dini kukemea siasa na uendeshaji mbovu wa mifumo ya serikali wakiwa kwenye huduma zao kuliko wakiingia ndani ya siasa na serikali ambako tumeona wakibezwa sana na mamlaka zao za kihuduma zikisongwa/zikitingwa na sintojuwa za mifumo iliyopo ya kuendesha nchi. Naamini watafanikiwa zaidi kuzishauri serikali wawapo kwenye huduma zao madhabahuni kuliko wakiwa ndani ya serikali hizo, bungeni na kwenye vyama vya siasa.
Ebu sasa tuone ushahidi wa nyakati hizi ambapo viongozi wa dini wameweza kwa ujasiri mkuu kuingilia kati na kuokoa hatima za nchi zao: Nchini Kenya Ask. John Henry Okulu wa CPK [Anglican] Dayosisi ya Maseno na Ask. Alexander Muge wa CPK Dayosisi ya Eldoret walivyotumia madhabahu zao vizuri kukemea na kusahihisha mwenendo wa siasa katika nchi yao.
Mch. Canaan Banana alipigania uhuru wa Zimbabwe hadi akaja kuwa Rais wa kwanza wa Zimbabwe huru, Ask. Pius Ncube amejitokeza hadharani na kusimama kidete kukosoa njia ambayo siasa za nchi yake zilichukuwa na kuifanya Zim kuwa kisiwa katika nchi kavu duniani na kuporomosha uchumi wa taifa [The highest inflation in the world “Hyperinflation”] na raia kuogelea kwenye umasikini.
Ask. Desmond Tutu sote tunajuwa mchango wa color yake ya kiaskofu na Biblia yake vilivyoleta ukombozi Afrika Kusini. Mchango wake uliongezea nguvu kubwa jitihada zilizopwaya za wanasiasa wapigania ukombozi. Kwa hivyo Watumishi wa Mungu wana kibali kuingilia masuala ya siasa kukosoa, kukemea, kuhoji, kurekebisha, kushauri na kuokoa pia. Tena wao ni bora zaidi kwa sababu hawafanyi kwa akili zao wenyewe bali wanafanya kwa karama zilizo ndani yao na kwa kumuuliza Mungu kwanza juu ya hali ya nchi/ufalme ili Mungu awape cha kufanya kwa hekima itokayo kwake.
Haiwezekani watu wanachunwa ngozi na kukatwa viungo na wengine wazee kuuawa kwa kudhaniwa ni washirikina eti tu kwa kuwa macho yao yamekuwa mekundu alafu viongozi wa dini wakijaribu kutathmini utendaji wa dola katika kuzuia uhalifu huu na mwingine uwao wote ule waambiwe kuwa wanaingilia siasa. Katiba ndiyo inalinda haki ya kila mtu kustahili kuishi wakiwemo watu wenye ulemavu wa ngozi, sasa viongozi wa dini wakijaribu kudurusu katiba ili iweze kuwa bora zaidi yenye kuwakilisha maslahi mapana ya jamii nzima wanaambiwa wanaingilia siasa. Labda tuaminishwe kwamba tunaishi zama za Herode na Pilato!
Wanasiasa wajuwe kuwa Mungu amewaagiza viongozi wa dini wahubiri watu kutoua, kutochuna ngozi, kutokata viungo na ukatili wa kila namna na Mungu atakuja kuwadai kuwa walihubirije agizo lake katika Mik.3:2-3 2Ninyi mnaoyachukia mema, na kuyapenda mabaya; ninyi mnaowachuna watu ngozi yao, na nyama mifupani mwao. 3Naam mnakula nyama ya watu wangu, na kuwachuna ngozi zao, na kuvunja mifupa yao; naam, kuwakata vipande vipande kama kwa kutiwa chunguni, na kama nyama sufuriani.
Pia tunasoma katika Mit.23:22 “Msikilize baba yako aliyekuzaa, wala usimdharau mama yako akiwa mzee.” Sasa wazee wanapouawa kwa tuhuma za macho kuwa mekundu kuwa ni wachawi na wanasiasa wapo lakini jitihada zao hazizai matunda kutokomeza ukatili huu, kwa nini viongozi wa dini wakiingilia kuhoji ufanisi wa utendaji wa wanasiasa wanatishiwa?
Ninawatia moyo viongozi wa dini kuwa wajichukulie kuwa wametumwa kuhubiri habari za Mungu kama kondoo katikati ya mbwa mwitu. Eze.2:6 “Na wewe, mwanadamu usiwaogope hao, wala usiyaogope maneno yao, ijapokuwa miiba na michongoma i pamoja nawe, nawe unakaa katikati ya nge; usiyaogope maneno yao, wala usifadhaike kwa sababu ya nyuso zao, wajapokuwa ni nyumba yenye kuasi.Tunaangamia kwa kukosa maarifa Hos.4:6.
Mbona viongozi wadini wanapojenga miradi ya maendeleo ya Kanisa kwa ajili ya jamii nzima huwa wanasiasa hawahoji kuwa kwa nini wanawaingilia kwenye kazi zao? Mbona hawahoji kuwa viongozi wa dini wanatekeleza ilani ipi ya uchaguzi? Mbona miradi ya maendeleo ya Kanisa ndiyo iliisimamisha nchi hata leo tangu uhuru? Wanasiasa hawa hawa wamejengwa kwenye shule za Kanisa. Wanasiasa wajuwe kuwa viongozi wa dini siyo wapinzani ambao hata wakifanya cha maendeleo ya umma katika majimbo yao bado watasukumwa sana. Bado tunakumbuka neti za hospitali ya Temeke zilivyopata tabu kukubalika miaka ileee zilipotolewa kama msaada na kiongozi mmoja wa upinzani katika jimbo hilo.
Je, wanasiasa wa Afrika wana utandu ulioziba mboni zao zisione hata mema? Mbona mauaji yanaposhindikana kutokomezwa kwenye jamii wanasiasa hao hao wanawaomba viongozi wa dini kuongeza bidii ya kufundisha Neno la Mungu ili jamii isiangamie na kuwa kama namna ya kujisafisha kwa wafadhili?
Bara la Afrika lisipothamini nafasi ya viongozi wa dini kama wadau wa msingi na muhimu sana katika kuendesha nchi na lisipofanya marekebisho ya mwenendo wa uendeshaji wake basi nachelea kusema maandiko haya yaweza kutimia:
Maombolezo.4:17 “Macho yetu yamechoka kwa kuutazamia bure msaada wetu; katika kungoja kwetu tumengoja taifa lisiloweza kutuokoa.”
Mhubiri.10:5-7 5Liko baa nililoliona chini ya jua, nalo ni kama kosa litokalo kwake yeye atawalaye: 6ya kuwa upumbavu huwekwa mahali pa juu sana, nao wakwasi hukaa mahali pa chini. 7Mimi nimeona watumwa wamepanda farasi, na wakuu wakienda kwa miguu juu ya nchi kama watumwa.”
Kwa hisani ya Majwala.

KAMA UNA MAONI YOYOTE NIANDIKIE HAPO CHINI AU TUMA UJUMBE KWENYE NO 0784 477775 au Whatup 0784 477775 AU FB Martin Malecela follow me in Twetter martmalecela au tembelea page yetu na ulike martmalecela.blogspot.com

Hakuna maoni: