Ijumaa, 27 Machi 2015

NDOA YAAYUBU WA SASA



 
Basi Shetani akatoka mbele za uso wa BWANA, akampiga Ayubu na majipu mabaya tangu wayo wa mguu hata utosi wa kichwa. Naye akashika kigae cha kujikunia; akaketi majivuni. Ndipo mkewe akamwambia, Je! Wewe hata sasa washikamana na utimilifu wako? Umkufuru Mungu, ukafe. Lakini yeye akamwambia, Wewe wanena kama mmoja wa hao wanawake wapumbavu anenavyo” (Ayubu 2:7-10). 
 
Katika kufuatilia kwangu habari za Ayubu, kuna jambo limenishangaza sana. Mke wa Ayubu alipoonekana kwenye kitabu cha Ayubu mlango wa 2, wakati anakemewa na mumewe, hakuonekana tena hadi milango ya mwisho ambapo tunasikia Ayubu alizaa tena wana na mabinti. Jambo jingine, katika habari zote za Ayubu, hakuna mahali nimeona akisimulia MATENDO ya mkewe kwake au kwa Mungu ila nimesikia akisema habari za WATOTO, MALI zake na watu wengine.
 
Wakati Ayubu anakumbukia maisha yake ya zamani kabla ya pigo la adui, ametaja mambo mengi anayoya-miss ila hakutaja mkewe! Ayubu anakumbuka jinsi watoto wake walivyozunguka meza yake (Ayubu 29:5), jinsi alivyokuwa na heshima yake kwa jamii inayomzunguka (Ayubu 29:7-10) na jinsi alivyotembea na Mungu wake (Ayubu 29:2-6), hakuna mahali ameeleza kwa UZITO jinsi alivyoishi kwa FURAHA na mkewe! Najiuliza, je! Ayubu alisahau kusema habari NZURI za mkewe au hazikuwepo?  Je! Kama alisahau, mbona hatuoni huyu mama akiketi majivuni na mumewe na kumkuna mgongoni kwa kucha zake hadi Ayubu anajikuna kwa kigaye? Je! Huyu mama hakuwa mfariji wakati wa MAPITO haya au alizira kwa sababu aliitwa ananena kama mwanamke mpumbavu huku mwanzo?
 
Nikatafakari tena nyakati na majira nikaona jambo jingine. Fikiri katika nyakati zetu (Ayubu angekuwepo sasa), baba anamwambia mkewe, “wewe umenena/tenda kama mmoja wao wa hao wanawake wapumbavu” kwa sababu kweli mkewe amenena jambo la kipumbavu lisilopaswa kunenwa au kutendwa kwa jamii ya waaminio! Fikiri huyu mama angejibu au kufanya nini? Kwa wakati wa Ayubu, kutafuta mwanaume mwingine maana yake ni kusaini hati ya kifo, yaani kupigwa mawe hadi kufa. Kwa hiyo, yamkini kilichomshika huyu mwanamke “mpumbavu” sio hofu ya Mungu wala upendo kwa mumewe ila ni hofu ya kupigwa mawe hadi kufa! Fikiri mke wa Ayubu wa sasa, piga picha ndani ya kanisa, wala usiangalie nje. Je! Unaona nini?
 
Ukitaka kujua habari ya nyakati na majira, angalia hapa, kuna kundi kubwa jingine la wapumbavu, ambao wana mfano wa utauwa, “ 1 Lakini ufahamu neno hili, ya kuwa siku za mwisho kutakuwako nyakati za hatari. 2Maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda fedha, wenye kujisifu, wenye kiburi, wenye kutukana, wasiotii wazazi wao, wasio na shukrani, wasio safi, 3wasiowapenda wa kwao, wasiotaka kufanya suluhu, wasingiziaji, wasiojizuia, wakali, wasiopenda mema, 4wasaliti, wakaidi, wenye kujivuna, wapendao anasa kuliko kumpenda Mungu; 5wenye mfano wa utauwa, lakini wakikana nguvu zake; hao nao ujiepushe nao. 6Kwa maana katika hao wamo wale wajiingizao katika nyumba za watu, na kuchukua mateka wanawake wajinga wenye mizigo ya dhambi, waliochukuliwa na tamaa za namna nyingi; 7wakijifunza siku zote, ila wasiweze kabisa kuufikia ujuzi wa kweli. 8Na kama vile Yane na Yambre walivyopingana na Musa, vivyo hivyo na hawa wanapingana na ile kweli; ni watu walioharibika akili zao, wamekataliwa kwa mambo ya imani. 9Lakini hawataendelea sana; maana upumbavu wao utakuwa dhahiri kwa watu wote, kama vile na upumbavu wa hao ulivyokuwa dhahiri (2 Timotheo 3:1-9).
 
Nimeangalia na kujifunza makundi mawili ya watu, wapo wamtafutao Mungu katika shida zao (wenye hekima na ufahamu) (Ayubu 28:28) na wapo wamwachao Mungu katika shida zao (wapumbavu) (Ayubu 2:7-10). Wakati Ayubu anazungumza juu ya hekima, alisema, “Kisha akamwambia mwanadamu, Tazama, kumcha Bwana ndiyo hekima, Na kujitenga na uovu ndio ufahamu(Ayubu 28:28). Je! Umeona janga kwenye kizazi hiki? Naam, bila shaka kama Mtume Paulo alivyosema juu ya nyakati, hizi ni siku za mwisho, utawaona siku zote wakijifunza habari za Mungu ila hawafikilii UJUZI WA KWELI! Je! Mtu aweza kufikilia ujuzi wa kweli bado akawaza kama mke wa Ayubu? Je! Mtu aweza kufikilia ujuzi wa kweli, akawa HURU na akaendelea kutenda DHAMBI hasa za makusudi? (Yohana 8:31,32).
 
Upumbavu maana yake ni kufanya jambo ambalo mtu ANAJUA kwamba ni MAKOSA na ANAFANYA kwa MAKUSUDI tu, huyu ni mpumbavu. Je! Umeona upumbavu katika jamii ya waaminio? Paulo anasema, “hawataendelea sana kabla upumbavu wao haujadhirika”. Huna haja ya kupambana na gugu, wewe mtu wa Mungu shika njia za BWANA na uzidi kuimarishwa kwa maana “waovu watazidi kuwa waovu na watakatifu watazidi kutakaswa” (Ufu. 22:11; 2 Tim. 2:16), haleluya!
 
Ukiona waovu wanazidi kuwa waovu, na uasi unaongezeka, hata wajuapo au waonywapo, jua saa imefika ya kuchunga roho yako na imani yako, usije ukakasirishwa na kutahayari na kisha kuharibu uhusiano wako na Mungu, kwa maana BWANA alituambia dalili za siku za mwisho, “Na kwa sababu ya kuongezeka maasi, upendo wa wengi utapoa. Lakini mwenye kuvumilia hata mwisho, ndiye atakayeokoka” (Mathayo 24:12, 13). Upendo kupoa ni dalili mojawapo ya kurudi nyuma. Bila shaka UVUMILIVU wako ndio utakuokoa!
 
Bwana anarudi,
 
kwa hisani ya Frank Philip Seth. 

KAMA UNA MAONI YOYOTE NIANDIKIE HAPO CHINI AU TUMA UJUMBE KWENYE NO 0784 477775 au Whatup 0784 477775 AU FB Martin Malecela follow me in Twetter martmalecela au tembelea page yetu na ulike martmalecela.blogspot.com

Hakuna maoni: