Alhamisi, 15 Januari 2015

KUUSHINDA ULIMWENGU



 
Kwa maana huku ndiko kumpenda Mungu, kwamba tuzishike amri zake; wala amri zake si nzito. Kwa maana kila kitu kilichozaliwa na Mungu huushinda ulimwengu; na huku ndiko kushinda kuushindako ulimwengu, hiyo imani yetu. Mwenye kuushinda ulimwengu ni nani, isipokuwa ni yeye aaminiye ya kwamba Yesu ni Mwana wa Mungu? [... ] Twajua ya kuwa kila mtu aliyezaliwa na Mungu hatendi dhambi; bali yeye aliyezaliwa na Mungu hujilinda, wala yule mwovu hamgusi” (1 Yohana 5:3-5, 18).
 
Kanuni ya kuushinda ulimwengu ipo katika mambo matatu: kuzaliwa na Mungu (yaani kuzaliwa mara ya pili kwa kumpokea Yesu kama BWANA na Mwokozi wa maisha yako), kumpenda Mungu (yaani kushika amri zake), na kujilinda (yaani kuangalia kwa BIDII kufanya sawa na Neno la Mungu pamoja na kusali na kuomba).
 
Kumekuwa na JITIHADA nyingi za watu kuepuka dhambi ambazo mwisho wake ni KUSHINDWA kila siku na kujiletea majuto na maumivu. Wapo wengi wamejitahidi kuwa WEMA kwa nguvu zao, kujiepusha na mambo fulani kwa nguvu nyingi, na hata wamejiwekea masharti fulani ili wasitende dhambi, mwisho wa siku wanajikuta wamefanya jambo lile lile wanalopingana nalo akilini mwao.  Ukiona hali hii inajitokeza, tena mara kwa mara, anza kujiuliza maswali, je! Umezaliwa na Mungu? Je! Unamtafuta Mungu kwa BIDII katika kusoma Neno & kutafakari, kusali na kuomba? Je! Unampenda Mungu?
 
Kwa bahati mbaya sana, kumpenda Mungu hakupo katika maneno, ila matendo yako. Angalia hapa “Yeye asemaye, Nimemjua, wala hazishiki amri zake, ni mwongo, wala kweli haimo ndani yake. Lakini yeye alishikaye neno lake, katika huyo upendo wa Mungu umekamilika kweli kweli. Katika hili twajua ya kuwa tumo ndani yake” (1 Yohana 2:4-5). Jiulize maswali haya: je! Unachukia uovu? Je! Unajiepusha na uovu? Kama majibu yako ni ndio, basi kwa kifupi wewe unampenda Mungu. Angalia mfano wa Yusufu akiwa kwa Potifa kule Misri (Mwanzo 39). Yusufu alijua kwamba angeweza kuzini na yule mama, mke wa Potifa na bwana wake asijue, ila alisema “nimtendeje Mungu dhambi kubwa namna hii?” Yusufu alijua shida sio kufumaniwa wala watu kujua, shida ni kumtenda Mungu dhambi. Kwa sababu Yusufu alimpenda Mungu sana, akashinda ile dhambi.
 

Sasa kuna jambo hili nataka ujifunze. Sio kwamba kila atendaye makosa au dhambi hampendi Mungu. Kuna tofauti ya kutenda dhambi na kuipenda dhambi.   Angalia hapa tena, “Msiipende dunia, wala mambo yaliyomo katika dunia. Mtu akiipenda dunia, kumpenda Baba hakumo ndani yake. Maana kila kilichomo duniani, yaani, tamaa ya mwili, na tamaa ya macho, na kiburi cha uzima, havitokani na Baba, bali vyatokana na dunia. Na dunia inapita, pamoja na tamaa zake, bali yeye afanyaye mapenzi ya Mungu adumu hata milele” (1 Yohana 2:15-17). Hali ya moyo wako ndiyo itakupelekea kujua kwamba unaipenda dhambi au la, usijidanganye na maneno matupu, kagua moyo wako na jiulize “hii kiu ya dhambi fulani inatoka wapi?”
 
Dalili ya mtu “anayependa dunia na mambo yake” ni KUDUMU katika dhambi fulani na KUIFURAHIA, na maana yake ni KUTOKUMPENDA Mungu. Ukiona unafanya dhambi, halafu haukwaziki wala kuumia ndani yako (hali ya majuto), inaonesha UNAIPENDA hiyo dhambi; ni vigumu kuiacha au kuiepuka, unahitaji msaada wa Mungu. Nikatazama tena jambo hili,  “…. bali yeye aliyezaliwa na Mungu hujilinda, wala yule mwovu hamgusi” (1 Yohana 5:18). Pamoja na neema, nakwambia kuna BIDII ya kumtafuta Mungu na mambo yake, na hiyo itakuokoa na mengi. Kadri unavyomtafuta Mungu na mambo yake unazidi kuonekana kwake. Wakati huo ukimtafuta Mungu kwa BIDII unajikuta na utu wako wa ndani unabadilishwa taratibu. Ghafla! Unajikuta unachukia dhambi, na unasikia kukosa amani ukifikiri tu habari ya kutenda dhambi hata kabla ya kuitenda, ukifikia hatua hiyo jua umeanza kumpenda Mungu.
 
Hatua za KUJILINDA ni hatua za MAKUSUDI kabisa na wala sio za kukaa tu, huku unatenda dhambi kwa kisingizio cha neema. Hizi hatua ndio zinaonesha KIASI cha imani yako, kwa maana imeandikwa “imani bila matendo imekufa nafsini mwako”. Hayo matendo ufanyayo katika harakati za kujilinda (kuepuka uovu), kama ilivyokuwa kwa Yusufu, inaonesha kiwango chako cha kumpenda Mungu wako na kumtii.
 
Inasikitisha sana kuona jinsi ambavyo watu wanahubiri, kufundisha na kushawishi watu kwa BIDII sana juu ya sadaka, ila ni wapole sana, au wanazungumza kwa ulegevu habari ya dhambi! Je! Kuacha kutoa fungu la kumi na uzinzi kanisani ni kipi cha kukemea zaidi?  Au kwa sababu “atendaye dhambi anawajibika kwa Mungu yeye binafsi, ILA atoaye fungu la kumi anawajibika kwa Mungu na kwetu pia?” na kwa maana hii, tumeweka BIDII katika sadaka kwa sababu nasi twafaidika? Angalia jambo hili, usiache kutoa sadaka zako, ila jilinde na uovu ili sadaka zako ziwe na maana mbele za Mungu, angalia mfano wa Korinelio (Matendo ya Mitume 10). Sadaka zako bila kuacha uovu, bado haimaanishi unampenda Mungu! “Tena nikitoa mali zangu zote kuwalisha maskini, tena nikijitoa mwili wangu niungue moto, kama sina upendo, hainifaidii kitu” (1 Wakorinto 13:3).
 
Frank Philip. 

KAMA UNA MAONI YOYOTE NIANDIKIE HAPO CHINI AU TUMA UJUMBE KWENYE NO 0784 477775 au Whatup 0784 477775 AU FB Martin Malecela follow me in Twetter martmalecela au tembelea page yetu na ulike martmalecela.blogspot.com

Hakuna maoni: