Jumatano, 7 Januari 2015

BWANA HAMSHANGAI ADUI, ILA ANAKUSHANGAA WEWE UKISHINDWA KATIKA VITA NA SHETANI


 
Ikawa siku zile mojawapo alipanda chomboni yeye na wanafunzi wake, akawaambia, Na tuvuke mpaka ng’ambo ya ziwa. Wakatweka matanga. Nao walipokuwa wakienda, alilala usingizi. Ikashuka tufani juu ya ziwa, chombo kikaanza kujaa maji, wakawa katika hatari. Wakamwendea, wakamwamsha, wakisema, Bwana mkubwa, Bwana mkubwa, tunaangamia. Akaamka, akaukemea upepo na msukosuko wa maji, vikakoma; kukawa shwari. Akawaambia, Imani yenu iko wapi? Wakaogopa, wakamaka, wakisema wao kwa wao, Ni nani huyu basi hata anaamuru upepo na maji, navyo vyamtii?” (Luka 8:22-25)
 

Kuna jambo limekaa moyoni mwangu siku nyingi, nalo ni habari ya majaribu au vita katika maisha ya imani. Jambo la msingi sana kujua ni kwamba “ulimwenguni tunayo dhiki”, BWANA anajua, na akasema “tujipe moyo kwa maana Yeye ameushinda ulimwengu” kwa hiyo “Aweza kuwasaidia na kuwaokoa wote wajaribiwao kwa sababu BWANA pia alijaribiwa katika KILA jambo” kama ilivyo sisi leo.
 
Mtume Paulo aliposema, “Nimevipiga vita vilivyo vizuri, mwendo nimeumaliza, Imani nimeilinda;   baada ya hayo nimewekewa taji ya haki, ambayo Bwana, mhukumu mwenye haki, atanipa siku ile; wala si mimi tu, bali na watu wote pia waliopenda kufunuliwa kwake” (2 Timothy 4:6,7), inaonesha kabisa kwamba Mungu aliruhusu VITA kwa makusudi ili PAULO apambane, na kuna TAJI baada ya USHINDI. Kwa upande mwingine, Paulo hakusema “ni kwa neema tu”, ila anasema “mwendo nimeumaliza, imani nimeilinda”, hii inanipa picha ya DHAMIRI ya dhati ndani ya Paulo ambayo ALIKUSUDIA kusimama katika MAPENZI ya Mungu kwa hali zote, “akifa ni faida, akiishi ni kwa sababu ya kazi ya injili”. Sihubiri kinyume na neema ya Mungu, ila nataka nikuoneshe umuhimu wa kutambua kwamba kila mmoja wetu anawajibu wa kusimama katika zamu zake na kufanya yampasayo japo hatuishi kwa sheri, na haki yetu haitahesabiwa kwa sheria, ila kwa imani. Ona mfano wa BWANA na wanafunzi wake chomboni, BWANA hakushangaa TUFANI kwa sababu imeleta vurugu pale, Aliwashangaa wanafunzi wake kwa kushindwa KUPAMBANA na tufani. Ona tena, BWANA akauliza, “imani yenu iko wapi?” Je! Utasema unaimani pasipo MATENDO? Kwanini basi kusema na kusingizia “neema tu” huku unishi maisha ya aibu na hutaki kubadilika? Je! Maneno yako matupu na “Bwana asifiwe” nyingi zaweza kukuokoa? Je! Uzidi kutenda dhambi ili neema iongezeke? La! Hasha. Acha njia zako mbovu na mrudie BWANA.
 
Ni kweli “tunalindwa na nguvu za Mungu kwa imani”, lakini imekupasa “kuomba bila kukoma” (yaani KUFANYA jambo), imekupasa “kumtafuta Mungu kwa bidii, na tukimtafuta kwa BIDII ndipo tunamwona JAPO hayuko mbali na yeyote kati yetu”.
 
Ona tabia hii, “Naye mwenyewe alikuwapo katika shetri, amelala juu ya mto; wakamwamsha, wakamwambia, Mwalimu, si kitu kwako kuwa tunaangamia?”  (Marko 4:35-41). Tabia ya kulaumu wengine au Mungu kwa kushindwa kwetu kusimama kwa imani. Ikitokea tufani watu wanaanza KUMLAUMU Mungu bila kujua kwamba huwezi kuwa mshindi kama hakuna mashindano! Vita sio jambo la kushangaa, kwa maana Mungu wetu jina lake ni “BWANA wa vita”, na yeye hutuacha tuingie vitani ili tuuone mkono wake ukituokoa huku “akijionesha mwenye nguvu kama mioyo yetu imemwelekea”, jicho la BWANA linakimbi-kimbia duniani mwote kwa kusudi hili, “kujionesha mwenye nguvu”, Je! Yupo mmoja aliye na uelekevu kwa BWANA asimwone mwenye nguvu? Kama Bwana ni mwokozi jua unahitaji akuokoe, na wokovu hauishii siku ile umesema sala ya toba, wokovu ni jambo la kuendelea, “kila atakayeliita jina la BWANA ATAokoka”. Mwite BWANA kwenye mambo yako akuokoe.
 
Lipo jambo jingine nimeliona, likanisumbua sana. Je! Umewahi kusikia mtu akisema, “nikihama mtaa huu, nitaweza kusimama katika wokovu”, au “kama isingekuwa huyu mke/mume, kiroho changu kisingekuwa hovyo namna hii”, nk., je! Umewahi kujiuliza kama waovu wote wanaondolewa duniani, changamoto zote zingeondolewa, Ibilisi amefungwa kamba milele, hakuna shida, pepo wala majaribu, je! Kungekuwa na haja gani ya kuwa na BWANA ambaye ni MWOKOZI? Je! Imani yako si itakuwa bure tu? Kwani watu au Mungu atajuaje kwamba unamwamini kama hakuna changamoto pande zote? Je! Unataka kusema “umeweza kusimama kwenye wokovu kwa sababu shida zako na changangamoto zimekwisha”? nataka nikwambie jambo hili, BWANA hashangai changamoto zako, ila anakushangaa wewe UKISHINDWA kusimama katika hizo changamoto na kuzishinda; kila ukijikwaa anakuuliza “imani yako iko wapi?”.
 
Jifunze jambo hili, hilo jaribu lako LITARUDIA na KUDUMU sana, hadi utakapolishinda, ndipo utavuka hatua zingine za imani; yaani ufike mahali pa KUMTII Mungu katika hiyo “tufani” yako, ndipo utasikia BWANA akisema juu yako, “watakatifu alioko duniani ndio wanaonipendeza”, kwa maana wanasimama katika njia za BWANA japo katika dhiki zao Ukisubiri Mungu aondoe changamoto zako ndipo usimame katika wokovu, hiyo siku iko mbali nawe kwa maana ni mapenzi ya Mungu tuingiapo katika majaribu na changamoto mbali mbali na imetupasa kumshukuru Mungu kwa mambo yote; na kushinda kwetu kunampa BWANA heshima na utukufu wa pekee, Anapenda kutuona tukishinda, ndio maana ameandaa taji kwa washindi wote.
 
Frank Philip.
 
KAMA UNA MAONI YOYOTE NIANDIKIE HAPO CHINI AU TUMA UJUMBE KWENYE NO 0784 477775 au Whatup 0784 477775 AU FB Martin Malecela follow me in Twetter martmalecela au tembelea page yetu na ulike martmalecela.blogspot.com

Hakuna maoni: