Jumatano, 30 Machi 2011

ABUDU MUNGU TU!!!!

KUTOKA KUMWABUDU MUNGU HADI KUABUDU KAZI.



Nachukua nafasi hii kumshukuru Mungu aliye hai kwa upendo wake usio na kikomo juu ya mwanadamu kwa kutupa neema ya kuishi mpaka sasa, pili kuwashukuru wale wote wanao fuatilia blog yangu Mungu awabariki sana. Nirudi kwenye mada yangu ya leo watu tuliookoka tuna pande mbili za maisha mambo ya Mungu na mambo ya kaisali na mambo yote haya ni ya muhimu sana katika maisha yetu ila kunatakiwa kuwa na ulinganifu wa utendaji ili tusijikute tumelalia upande mmoja. kipindi tulichonacho kimekuwa cha hatari sana kiasi kwamba tusipokuwa makini katika kristo utajikuta umepoteza lengo kabisa katika maisha ya wokovu na ndiyo maana kila mtu ukikaa nae atakueleza habari za zamani na si za sasa kuwa enzi zetu bwana tulikuwa tunafunga sana, au tunaomba sasa au kuimba sana n.k, swali la kujiuliza je? kwasasa hivyo vitu hatutakiwi kuvifanya au tunashindwa kuvifanya, kwa hiyo basi utagundua kuwa kuna vitu tumepoteza baada ya kuukulia wokovu watu wameuzoea wokovu na wamedumaa na hofu ya Mungu imetoweka kabisa mioyoni mwao hii imesababisha kuwa na mapooza kanisani watu wazito wanapenda ishara kuliko kitu chochote bila kujua kuwa mambo ya Mungu yanahitaji gharama tena sio ndogo usipolipa gharama utaishia kusikia miujiza kwa watu wengine na unaweza ukadhania kuwa Mungu hana upendeleo kumbe watu umetoka kwenye msitari tunapishana na Baraka na ahadi za Bwana.


Tuangalie maandiko machache Mungu anatutaka tufanye nini. KUT 20:3 – 6 Usiwe na miungu mingine ila mimi, usijifanyie sanamu ya kuchonga, wala mfano wa kitu chochote kilicho duniani. Usivisujudie wala kuvitumikia, kwa kuwa mimi Bwana Mungu wako ni Mungu mwenye wivu, nawapatiliza wana maovu ya baba zao, hata kizazi cha tatu n cha nne cha wanichukiao, nami nawarehemu maelfu elfu wanipendao, na kuzishika amri zangu. MAT 6:31 – 34 Msisumbuke basi mkisema tule nini? Au tunywe nini? Au tuvae nini? Kwa maana hayo yote mataifa huyatafuta, kwasababu baba yenu wa mbinguni anajua ya kuwa mnahitaji hayo yote. Bali utafuteni kwanza ufalme wake na haki yake na hayo mengine mtazidishiwa. Basi Msisumbukie ya kesho kwa kuwa kesho itajisumbukia yenyewe yaosha kwa siku maovu yake. Maandiko hapo juu kwanza inaonyesha jinsi Mungu alivyo na wivu juu yetu wanadamu tuliokoka hataki kabisa kumwabudu mungu mwingine ila yeye peke yake wala hataki tumchanganye na kitu kingine chochote tuwe kwake 100 % hapendi michanganyo ukimchanganya yeye anasema atatutapika hatutakiwi kuwa vuguvugu, anataka abakie yeye peke yake ili anapofanya mujiza na ijulikane ni yeye amefanya na si vinginevyo Wam 7:2 wivu huu wa Mungu ni mkubwa mno kuliko hata ule watu wanaokuwa nao kwa waume/wake zao na inaonyesha kuwa yeyote asiyekwenda sawa na neno hili hasira ya Bwana itawaka juu yake na familia yake. Swali lakujiuliza kweli watu tunasoma neno na kuelewa kile Mungu alichomaanisha kwetu? hapa mimi nina shaka kuwa wako ambao huwa hawalielewi neno kabisa japo wanalisoma kila siku suluhu sio kusoma biblia kila siku ila ni kuisoma kutafakari na kuieleewa kuwa Mungu anataka ufanye nini kama Danieli alivyoelewa na kufanyia kazi maandiko Dan 9:1 – 3 maana kama mtu atalielewa andiko, utaona litambadilisha katika maisha yake atafanya kama neno linavyomtaka (utawatambua kwa matendo au matunda yao) unaweza usinielewe kwa sasa namaanisha nini ila soma mpaka mwisho utanielewa na nina amini utapona juu la hili. hivyo kwa maana nyingine Mungu anataka tuwe kwake 100% na si vinginevyo na tunatakiwa kulifuata na kuliamini neno lake 100% na si vinginevyo lakini siku za leo imekuwa ndivyo sivyo mambo yamekuwa ni kinyume kabisa na neno la Mungu, na wewe mwenyewe utakuwa shahidi wa kwanza juu ya hili na kwa tatizo hili imesababisha kutokuwa na udhihirisho wa nguvu za Mungu katika maisha yetu au kanisa, Roho Mt anahudhunika maana anaona imani yetu imechakachuliwa na shetani watu wanaamini zaidi mambo yanayoonekana kuliko yale ya Mungu yanayo hitaji imani yasiyoonekana kwa macho ya nyama. Ebr 11:1


Andiko la pili la Mathayo ni jepesi kulitamka, kulikariri na hata kuliimba tatizo liko kwenye kulitenda hivi kweli tunatafuta kwanza ufalme wa Mungu? Au kuna vitu tumevifanya kuwa vya kwanza na ufalme wa Mungu umekuwa wa mwisho jibu unalo mwenyewe. Na je? Hatuyasumbuki ya kesho? Hapa jibu ni rahisi sana kuwa tunayasumbukia na ndiyo maana watu wako busy kutafuta mkate na maisha ya kesho na wengi wako kwenye mtego huu wa shetani na kuwa washirika wa jumapili kwa mwendo huu tutakuwa na nguvu za kumshinda shetani kweli!! au ndo unakuwa mfuasi wake? Nirudi kwenye kichwa changu cha habari kuwa watu wengi sasa hivi hawako kumwabudu Mungu ila wanamwabudu mungu kazi. kabla sijaingia kwa kina nitoe tahadhali kuwa sisemi watu wasifanye kazi ila unatakiwa kujua ni kitu gani kinachukwa nafasi ya kwanza katika moyo wako au muda wako mwingi ni Mungu au kazi jibu unalo. Niliona sehemu moja wamenyambulisha maana ya BUSY ni Be Under Satan Yoke ( kuwa chini ya utumwa au nira ya shetani) imekuwa fasheni kila mtu anasema yuko busy, mwanafunzi yuko busy, wainjilisti wako busy, wachungaji wako busy Hag 1:5 – 11. Hapa kazi ipo na tunahitaji neema ya kristo tu kututoa huko, imefanya watu kwenda kinyume na neno la Mungu. biblia inasema kwenye kitabu cha Yosh 1: 7 uangalie kutenda sawasawa na sheria yote aliyokuamuru Musa mtumishi wangu. Kumbe tunatakiwa kufuata sheria za Mungu sawasawa ili tufanikiwe katika Mungu usipoifuata sawasawa hapo lipo tatizo. Nimejaribu kufuatilia maisha ya watu katika pande 2 yaani upande wa Mungu na upande wa Kazi nimegundua yafuatayo watu wako tayari kufanya lolote atakayo ambiwa na bosi wake ili wasipoteze kazi zao hata kama mambo hayo mlokole hatakiwi kuyafanya yeye atafanya tu ili asimwage unga na kufuata sheria za kazi zote bila kupuuzia hata moja (Job description) kama unatakiwa kufika kazini saa moja mtu yuko tayari kufika saa moja kasoro robo kama anatakiwa kutoka saa 11 ataongeza na saa za ziada ili apate OT ili mradi bosi afurahie uwepo wake kazini lakini kwenye upande wa pili wa Mungu, watu hatufuati kabisa taratibu za kanisa na ibada utakuta ndiyo wa kwanza kuchelewa, kusinzia wakati wa ibada, na ni wakwanza kutoka hata ibada haijaisha, ibada za katikati ya wiki, zone na kwenye idara za kanisa ndo hawaonekani kabisa ukimuuliza atakuambia kuwa alichoka sana jana kazini alikuwa busy (duh kazi kubwa kuliko Mungu) ni wachache sana ambao wanaweza kufunga biashara zao au kuomba ruhusa kazini ili awahi kanisani, ukigusa michango hatoi unaweza kujiuliza huyu mtu kwani yuko busy for nothing!!! kama yuko for something basi atoe hata michango basi kazi ya bwana isonge mbele hatoi!!!. kwa hiyo hapa utaona kuwa watu wanatumikia na kusumbukia zaidi maisha yao kuliko Mungu mtu anayefanya hivyo ujue atategemea akili zake na si Mungu yaani tumemfanya Mungu kama mjomba vile heshima (hofu) ya Mungu makanisani imeshuka watu wanafanya hekalu la Mungu (kanisa) kama nyumba ya wanyanganyi hakuna tena hofu na nyumba ya Mungu watu wanaheshimu ofisi na nyumba zao kuliko nyumba ya Mungu.


Maisha au mahusiano yetu na Mungu yanaunganishwa na vitu vitatu navyo ni


• Kusoma neno la Mungu na kulielewa na kulitendea kazi


• Maombi na maombezi


• Kuwa na muda wa ibada (fellowship na Mungu)


Mambo hayo yakikosekana kwako ujue maisha yako ya wokovu yako hatarini sana na shetan anajua umuhimu wa hayo mambo 3 anachofanya uwe BUSY ili ukose muda wa kusoma neno , kuomba na ibada anajua usiposoma neno utakuwa huna maarifa ya neno la Mungu Hos 4:6 kwa upande mwingine hutakuwa na msingi mzuri hivyo unaweza kubadilishwa na mambo mengine, vilevile usipokuwa na maombi moto au nguvu ya roho mtakatifu itaisha ndani yako na mwisho anakubana usipate muda wa ibada na anakumaliza taatibu wewe utajua umesimama kumbe ulisha anguka zamani nafikiri mpaka hapa unaanza kunielewa na utakuwa na majibu mazuri kuwa Mungu ni nani kwako kazi au…………..


Labda nikuorodheshe baadhi ya mambo machache ambayo yako kwenye neno la Mungu wewe utajitathimini mwenywe.

 UNATAKIWA KUFANYA/KUTOFANYA SOMA ANDIKO JITATHIMINI MWENYEWE


1 Mizaha,kutenda haki, kutokua katika njia ya wakosaji. Zab 1:1


2 Kutokulipa baya kwa baya, kumpa aombaye na akopae Math 5:38 - 42


3 Tamaa za mwili. Wag 5:19 - 21


4 Kuukomboa wakati Waef 5: 16


5 Kusoma neno Wakol 3: 16 – 17


6 Kufurahi siku zote, Kushukuru siku zote Kujitenga na ubaya 1 The 5: 16


7 Kutafuta amani,utakatifukwa bidii Wabr 12: 14


8 Kuwa mtendaji wa neno Yako 1:22


9 Kutomwibia Mungu Mal 3:8 - 10


10 Kutomtegemea mwanadamu Yer 17:5

Yapo mambo mengi ila hayo ni baadhi tu fanya neno la mungu liwe kioo chako maana ibilisi anacho fanya ni kupofusha fahamu zetu ili kuto kuomba,kusoma na kutoelewa neno la Mungu na mapenzi ya mungu watu wamekuwa wapumbavu katika neno la Mungu Math 7:26 Na kila asikiaye haya maneno yangu na asiyafanye, atafananishwa na mtu mpumbavu, aliyejenga nyumaba yake juu ya mchanga. Sasa usikubali kuwa mpumbavu ili ibilisi asipate nafasi ya kukurubuni, baada ya kiroho kukuua viroho ndio kwanza vinashuka. Unashanga mtu ana muda mrefu kwenye wokovu lakini maisha yake ya wokovu hayaeleweki yani yupoyupo tu, nashukuru kuwa Roho mtakatifu aliliona toka zamani UFU 2:4 – 5 unasema. Lakini nina neno juu yako, ya kwamba umeuacha upendo wako wa kwanza. Basi kumbuka ni wapi ulipoanguka ukatubu ukafanye matendo ya kwanza. Lakini usipofanya hivyo naja kwako name nitakiondoa kinara zako katika mahari pake. Tusiache hasira ya Bwana iwake juu yako na maadamu uliokoka mwenyewe usitake kusukumwa sukumwa Yesu alisema kila anayetaka kunifuata ajitwishe msalaba wake na anifuate . maisha ya wokovu yana changamoto nyingi sana usipokuwa makini utaabudu kazi,biashara,masomo na kumwacha Yesu kabisa.
Leo niishie hapo ni maombi yangu kuwa Roho alifunue neno hili zaidi kwako na likazae matunda ambayo yeye amekusudia. Ubarikiwe sana tukutane kwenye somo jingine.


Hakuna maoni: