Ijumaa, 2 Januari 2015

FAHAMU UNDANI WA VITA KATI YA ISRAEL NA PALESTINA KIBIBLIA. ISRAEL ALIPEWA YAKOBO NA SI YAKUB. MPENDWA ENDELEA KUIOMBEA ISRAEL

Na Douglas Majwala
K
atika makala hii ya mafundisho ninawaletea hoja ngumu nzito zenye kuhitaji tafakuri, utulivu na umakini wa kutosha kuelewa mgogoro huu mkongwe duniani wenye mwanzo lakini unaonekana hauna mwisho, lakini wenye asili yake katika Agano la Kimbingu. Mimi binafsi nimelazimika kufanya maombi kabla ya kuanza kuandaa makala hii ya mafundisho; jambo ambalo ni nadra katika uandishi. Nikusihi na wewe mpenzi msomaji sasa utwae shajala zako [stationery] kama kalamu na note book au daftari lako na Biblia yako pia unapoanza kusoma mafundisho haya ambayo wengi wanayaonea aibu au hawana ujasiri wa kuyafunua wazi kwa umma ijapo wanafahamu ukweli wake katika maandiko, labda kwa kuogopa gharama za mahusiano na upande wa pili wa imani.



Lakini ajabu ni kwamba licha ya Biblia kuwa wazi kuhusu nani ni mmiliki halali wa maeneo husika hasa Yerusalemu lakini ni mara chache sana au hakuna kabisa maandiko haya kufundishwa au kuhubiriwa madhabahuni. Mimi mwenyewe ninakiri kuwa toka tumboni mwa mama yangu sijawahi kusikia habari hii iliyoandikwa kwenye Biblia ikihubiriwa au ikifundishwa kwenye madhabahu za Kanisani, semina na mikutano ya Injili. Katika kuandika makala hii, ninafanya hivi nikijuwa pia kuwa ninajitoa muhanga kufikisha ujumbe huu mahsusi kabisa wa mgogoro ambao umegharimu amani ya dunia, umegharimu amani ya Kanisa la MUNGU alilolinunua kwa damu yake mwenyewe Mdo.20:28, umegharimu rasilimali za dunia katika kuandaa mikutano ya kuuongelea na zaidi umegharimu roho za wahanga wa pande mbili husika.

Madai ya Wayahudi juu ya ardhi hii yanaegemezwa kwenye ahadi ya Kibiblia kwa Ibrahimu na kizazi chake, juu ya ukweli kwamba ardhi hii ilikuwa ni alama ya kihistoria ya falme za zamani za Kiyahudi za Israel na Yudea, na juu ya uhitaji wa Wayahudi kupata hifadhi salama dhidi ya Wakoloni wa Ulaya waliopingana na mila na desturi zao. Waarabu wa Kipalestina wanaegemeza madai yao kwenye kuendelea kuishi katika ardhi hiyo kwa maelfu ya miaka na ukweli kwamba waliwakilisha idadi kubwa ya watu hadi mwaka wa 1948. Wanakataa madai kuwa kuwepo ufalme wa nyakati za Kibilia hakuhalalishi madai ya nyakati za leo. Kama Waarabu wakihusisha madai ya Kibiblia, wanasisitiza kuwa madhali mtoto wa Ibrahimu aitwaye Ishmail ni baba mwanzilishi wa Waarabu, basi ahadi ya MUNGU ya kumilikisha ardhi hiyo kwa watoto wa Ibrahimu inaunganisha pia Waarabu kwa sababu Ishmail ambaye ni baba mwanzilishi wa Waarabu ni mtoto wa Ibrahimu huyo ambaye MUNGU anamilikisha ardhi hiyo kwa watoto wake. Hawaamini kwamba wanastahili kuachia ardhi yao kuwa fidia kwa Wayahudi kwa uhalifu uliotendwa na Wakoloni wa Ulaya kwa Wayahudi.

Naomba niweke wazi kuwa sitaongelea mikataba ya kisiasa kama ya Camp David, Roadmap and the Quartet, The United Nations Partition Plan ya Novemba 29, 1947 iliyogawa Wapalestina katika dola mbili za Wayahudi wa Palestina na Waarabu wa Palestina, wala sitaongelea vita ile ya mwaka 1949 baina ya Israel na dola za kiarabu vilivyoishia kuingia mkataba wa kuigawa Palestina katika dola tatu wakapewa Israel, Misri na Jordan; dola la Kiarabu la Palestina halikutambuliwa na mkataba wa mgawanyo huu wa UN; mkataba tata uliozaa vita vya 1947–1949 na kuzaa wakimbizi wa Kipalestina wapatao 700,000 waliokimbilia Israel ambapo Israel iliwabakisha Wapalestina 150,000 wenye asili ya Kiarabu na kuwafanya kuwa raia wa Israel na Israel ikawapa uraia wa daraja la pili na kuwekwa chini ya utawala na udhibiti wa kijeshi huku wakikosa haki za msingi kabisa kama raia na hawa ndiyo walikuja kuzaa kikundi cha Hamas ambao kwa kitendo cha kuwekwa chini ya mamlaka na udhibiti wa jeshi la Israel, walipata mianya ya maarifa ya kivita na Israel haikupata maono kuwa hawa siku moja watarudi na kuigeuka Israel kama tunavyoona sasa Hamas ikiongoza Palestina baada ya kurudi huko kwao kufuatia mikataba ya kisiasa isiyo na tija kutoa fursa ya kubadilishana wakimbizi ambao wengine wao kama hawa, walijikuta Israel kufuatia mgawanyo wa eneo lililogombewa kwa njia ya vita mwaka1947–1949.


Wala sitaongelea vita ya Juni 1967, pia sitaongelea azimio namba 242 la baraza la usalama la UN, ambalo pia ni azimio tata kwa sababu lilitoa agizo kwa Israel kuachia maeneo iliyoyateka katika vita hiyo na kutoa haki kwa dola zote zinazohusika na eneo hilo. Hili ni azimio tata kwa sababu tafsiri yake katika lugha ya Kifaransa inasema Israel inapaswa kuondoka katika maeneo hayo huku tafsiri ya lugha ya Kiingereza ikitoa mwito wa kuondoka kwenye maeneo hayo [Kifaransa na Kiingereza zote ni lugha rasmi za UN].

Israel na Marekani zinatumia tafsiri ya Kiingereza kubisha kuwa Israel iondoke kwenye baadhi tu ya maeneo lakini siyo maeneo yote ili kukidhi matakwa ya azmio hilo. Kwa miaka mingi Palestina iliendelea kukataa azimio hilo kwa kuwa halitambui uwepo wa utaifa wa Palestina na wakataka wakimbizi kupewa makazi ya haki ambako hawatasumbuliwa lakini zaidi kuwa azimio hilo lililotaka utambuzi wa kila dola katika eneo husika, linatoa mwito kwa Palestina kutambua Israel bila Israel kutambua haki za kitaifa za Palestina. Sitaongelea pia The October 1973 War and the Role of Egypt, wala sitaongelea mikataba ya Oslo, sitaongelea The 2002 Arab Peace Plan, sitaongela pia Palestinian Statehood and the UN.

Ifahamike kwamba mikataba hiyo yote haijazaa matunda tarajali. Makatibu Wakuu wote wa UN wamekuta mgogoro, wamejaribu kuutanzua na wakastaafu wakauacha ungali mbichi. Katika kutambua yote yaliyojiri kwenye mgogoro huu ambao mimi binafsi nimekuja duniani nikaukuta uliishakuwepo kwa miongo mingi, naomba nitoe azimio la kuwa na maslahi [declaration of interest] na upande wa Israel kwa sababu za ushahidi wa maandiko ya kitabu kitakatifu cha Biblia, na pia nikizingatia ukweli kuwa siwezi kutangua Agano la MUNGU aliloliweka na taifa lake la Israel [ambalo hata YESU mwenyewe hakulitangua], lakini zaidi nikiheshimu agizo la MUNGU la baraka na laana juu ya mtu awaye yote atakayeibariki au kuilaani Israel.

Lakini ni budi watu wote wakafahamu kuwa asilima kubwa ya usuluhishi wa kesi/migogoro chini ya jua huwa kanuni inayotumika siyo ya kutoa haki sawa kwa pande zote [Win-win situation badala yake ni kanuni ya Zero-sum ndiyo inatumika]. Ni Mbinguni tu ndiko kuna kanuni ya Win-win lakini chini ya jua kanuni ni Zero-sum kwa asilimia kubwa ya migogoro, na kwa hiyo napata ujasiri wa kusema kuwa suala la Mashariki ya Kati kanuni ya utatuzi wake lazima iwe ni Zero-sum ambapo mmoja akose na mmoja apate. Vinginevyo dunia itaendelea kushuhudia mashindano ya silaha na mbinu za kivita katika uwanja wa mapambano huku vikao vya kimataifa vya meza za duara vikiendela kupamba vyombo vya habari kwa ripoti za maazimio yanayoendeleza tu uhasama.

Ni bahati mbaya kuwa historia ya eneo linalogombewa haiainishwi wazi wazi [inafichwafichwa tu] kwa sababu ambazo nafikiri ama ni za uoga tu au ni za maslahi vikundi na hii inazidi kurefusha mgogoro huu. Nitajitahidi kudurusu historia kwa ushahidi wa maandiko. Ni katika mkondo huu wa uelewa [school of thought] wa muktadha wa jambo hili, kwamba tutaweza kubashiri mustakabali na hatima yake.

Lakini ili kujuwa kuwa maeneo yanayogombewa [Ukanda wa gaza, Yerusalemu na Ukanda wa Magharibi wa mto Yordani ambayo yote haya yako kwenye nchi ya ahadi ya Kibiblia ya Kaanani  ambayo ndiyo Israel ya leo, ambapo waliishi watoto wa Kaanani Mwa.10:15-18 ambao ni Sidoni, Hethi, Myebusi, Mwamori, Mgirgashi, Mhivi, Mwarki, Msini, Mwarvadi, Msemari, Mhamathi] na mpaka wa Wakanani ulianza kutoka Sidoni kwa njia ya Gerari hata Gaza Mwa.10:19. Kwanza ni budi tujuwe Kaanani ni nani? Mwa.10:1,6 inadhihirisha kuwa Kaanani ni mjukuu wa Nuhu kupitia mtoto wa Nuhu aitwaye Hamu. Hapo pia utagundua siri ya ajabu sana kuwa hata Misri ni jamaa katika ukoo wa Nuhu [sasa ardhi ya Misri nayo kwa mujibu wa Biblia ni ya Waisraeli, kwa maana hata Ishmail ni mtoto wa Ibrahimu kupitia kwa mjakazi Hajiri Mmisri, kwa hiyo Ibrahim alimposa Hajiri ambaye anatoka katika ukoo wa Nuhu kupitia kwa mtoto wa Nuhu aliyeitwa Hamu ambaye tumeona ni baba wa Kaanani]. Kwa mujibu wa mafungamano ya koo hizi za Kaanani ni dhahiri kuwa Mpalestina [ambaye ana mafungamano makubwa ya kisiasa, kidini na mila/utamaduni na nchi ya Misri ni Mmisri pia kupitia uarabu wao, Misri ndiyo chimbuko la uarabu] kwa vigezo hivyo ndani ya mabano anatoka katika ukoo mmoja na mzee Kaanani na katika ardhi moja ya Kaanani [ambako ndiko Israel ya leo pia, ambayo ndiyo nchi ya maziwa na asali na nchi ya ahadi, nchi ya Agano] kwa maana kwa mujibu wa Mwa.10:6, Misri na Kaanani ni watoto wa Hamu na ni wajukuu wa Nuhu.

Mvutano uliopo unatokana na ukweli kwamba hizi koo zilikuja kutawanyika Mwa.10:18,32 wengine baada ya gharika na ule msitari wa 31 unasema kuwa hata Shemu ambaye ni ndugu yake Kaanan kwa Nuhu, walikuja kugawanyika katika lugha zao, katika nchi [ardhi] zao na wakafuata mataifa yao. Sasa MUNGU anapotoa ahadi kuwa nchi yao anawapa Wayahudi/Waisrael; wanakuwa hawaelewi lugha anayoongea MUNGU ambaye ndiye mwenye ardhi hiyo kwa sababu yeye ndiye aliyeiumba kwa mikono na utashi wake, na vitu vyote ni vya kwake Zab.24:1na sawa na mzazi anapogawa urithi kwa watoto huwa hakuna anayeweza kumpangia kinyume na matakwa yake maana ardhi ni yake na watoto ni wake pia, na sababu kubwa ya wao kutoelewa lugha na iliyofanya nchi yao wapewe Wayahudi/Waisraeli ni kuwa walijiingiza kuabudu miungu wakamwacha MUNGU wa Israel ambaye ndiye MUNGU wa kweli, na MUNGU wa Israel mwenye wivu alipoona miungu inaabudiwa; alijitenga nao na alipojitenga nao ile nguvu  ya MUNGU iliyokuwa ndani yao wakati anawapa hiyo nchi [kabla hawajageukia miungu] ilihama ikaenda kwa Wayahudi/Waisrael na kutoa mwanya kwa Wakaanan, Sidoni, Hethi, Myebusi, Mwamori, Mgirgashi, Mhivi, Mwarki, Msini, Mwarvadi, Msemari, Mhamathi kuwa wadhaifu kwa kiwango cha kutomudu vita iliyoweka Kaanan katika milki ya Waisrael na ndiyo maana hata leo Palestina ambaye ametoka katika ukoo dhaifu uliopungukiwa na nguvu za MUNGU kutokana na uasi wa kugeukia miungu ameendelea kukosa nguvu na ushindi kila vita vinapoibuka dhidi yake na Israel ambaye nguvu za MUNGU zilihamia kwake.

Mgogoro kati ya Waarabu wa Kipalestina na Wazayoni [Israeli] ulianza kama mapambano kuhusu ardhi. Kuanzia mwisho wa vita kuu ya pili ya dunia hadi  mwaka 1948, eneo ambalo makundi yote mawili yalidai milki yake yalijulikana kimataifa kama Palestina. Jina hilo moja pia lilitumiwa kuelezea eneo ambalo halikutambulika sana “Ardhi Takatifu” na dini tatu za monotheistic [Mungu mmoja]. Kufuatia vita ya mwaka 1948–1949, ardhi hii iligawanywa katika maeneo matatu: dola la Israel, Ukingo wa Magharibi [wa mto Yordani] na Ukanda wa Gaza. Ni eneo dogo la wastani wa maili za mraba 10,000 au takriban ukubwa wa jimbo la Maryland nchini Marekani, kwa mujibu wa Middle East Research and Information Project ya Washington DC.

Ebu tafakari juu ya miujiza ambayo Israel inapata inapokwenda vitani huwa inatokana na uwezo wa kibinadamu kweli au uwezo wa MUNGU? Dunia inapaswa kujiuliza kuwa iweje kila vita vikilipuka hata ambavyo dunia nzima ya Waarabu wakiungana pamoja lazima Israel ishinde? Iweje Israel inapomaliza vita huwa haitetereki kiuchumi? Iweje mataifa makubwa duniani yanaogopa kuitenga Israel? Iweje Israel imudu kupiga hatua ya kimaendeleo na usalama hata pale ambapo inawekewa vikwazo vya kiuchumi na jumuiya za kimataifa na kubaki kama kisiwa? Iweje Marekani dola kubwa duniani ni mwepesi kuliwekea taifa lolote duniani vikwazo ikiwemo Urusi hata bila kupitia UN wakati fulani, lakini Marekani hiyo hiyo haithubutu kuiwekea Israel vikwazo ila itaiachia UN ifanye hivyo?

Itaendelea ambapo nitadurusu maandiko kadhaa yanayoonyesha jinsi MUNGU anavyotamka waziwazi kuwa ardhi hiyo inayogombewa amewapa Waisrael na kwamba maadui zake [Waarabu] hawana chao katika eneo hilo. Tena zaidi nitawapeleka kuona jinsi MUNGU anavyoagiza Israel kuwashughulikia kwa kulipiza maadui zake hao wanapomshambulia, hapa MUNGU anatumia lugha kali kabisa isiyo na huruma hata kidogo, na kwa vile ni maandiko ambayo lazima yatimie, ndiyo maana tunaona Israel ikishambulia maadui zake kwa viwango vya kutisha kabisa.   

KAMA UNA MAONI YOYOTE NIANDIKIE HAPO CHINI AU TUMA UJUMBE KWENYE NO 0784 477775 au Whatup 0784 477775 AU FB Martin Malecela follow me in Twetter martmalecela au tembelea page yetu na ulike martmalecela.blogspot.com

Hakuna maoni: