Jumatatu, 21 Desemba 2015

KWA NINI KUISOMA BIBLIA NA KUIELEWA?

Image result for bible picture

“Biblia ni kitabu cha dini kinachojulikana sana. Hata hivyo, ni kitabu cha kigeni na hakiwafai Wachina.”—LIN, CHINA.
“Hata vitabu vitakatifu vya dini yangu ya Kihindu sivielewi. Nitawezaje kuielewa Biblia Takatifu?” —AMIT, INDIA.
“Ninaiheshimu Biblia kwa kuwa ni kitabu cha zamani na nimesikia kwamba kimeuzwa zaidi kuliko vitabu vingine. Lakini, sijawahi kuiona.”—YUMIKO, JAPANI.
Watu wengi ulimwenguni wanaiheshimu sana Biblia. Hata hivyo, wengi wao hawajui yaliyomo katika Biblia. Hali iko hivyo kwa mamilioni ya watu wanaoishi barani Asia na hata katika nchi nyingi ambazo watu wengi wana Biblia.
Mwanamke akisoma Biblia
Huenda ukajiuliza hivi, ‘Kwa nini ninahitaji kuielewa Biblia?’ Kujifunza kuhusu kitabu hicho kitakatifu kunaweza kukusaidia:
  • Uridhike na uwe na furaha
  • Ushughulikie matatizo ya familia
  • Ukabiliane na mahangaiko
  • Uwe na uhusiano mzuri na watu
  • Utumie pesa kwa hekima
Mfikirie Yoshiko, anayeishi Japani. Alitaka sana kujua Biblia ina ujumbe gani, hivyo akaanza kuisoma. Matokeo yalikuwa nini? Anasema hivi: “Biblia imenisaidia kupata kusudi maishani na tumaini la wakati ujao. Sasa nimeridhika.” Amit aliyetajwa mwanzoni aliamua pia kuichunguza Biblia. Anasema: “Nilishangaa. Biblia ina habari zinazomfaa kila mtu.”
Biblia imeboresha sana maisha ya watu wengi. Kwa nini usiichunguze uone jinsi inavyoweza kukunufaisha?

Kitabu Kinachoeleweka

Kwa kweli, Biblia ni kitabu cha kale. Kina umri gani? Biblia ilianza kuandikwa miaka 3,500 hivi iliyopita huko Mashariki ya Kati. Kipindi hicho utawala wenye nguvu wa ukoo wa Shang ulikuwa ukitawala nchini China na karne kumi hivi baadaye dini ya Budha ilianza nchini India.
 
Biblia inatoa majibu yenye kuridhisha ya maswali muhimu sana kuhusu maisha
Ili kitabu kiwanufaishe na kuwasaidia watu, lazima kieleweke na kuwafaa. Ndivyo ilivyo Biblia. Inatoa majibu yenye kuridhisha ya maswali muhimu sana kuhusu maisha.
Kwa mfano, umewahi kujiuliza, ‘Kwa nini tuliumbwa?’ Swali hilo limewasumbua wanadamu kwa maelfu ya miaka, na bado linawasumbua. Hata hivyo, jibu la swali hilo linaweza kupatikana katika sura mbili za kwanza za kitabu cha kwanza cha Biblia, kitabu cha Mwanzo. Simulizi la Biblia katika sura hizo linaanza na “mwanzo,” yaani, mabilioni ya miaka iliyopita, wakati ulimwengu wetu unaotia ndani nyota na dunia ulipoumbwa. (Mwanzo 1:1) Kisha simulizi hilo linaeleza hatua kwa hatua jinsi dunia, viumbe mbalimbali, na wanadamu walivyoumbwa na pia kwa nini vitu hivyo vimeumbwa.

KITABU KINACHOELEWEKA

Biblia inatoa ushauri unaotusaidia kutatua matatizo ya kila siku. Ushauri huo unaeleweka kwa urahisi. Kuna mambo mawili yanayofanya ushauri wa Biblia ueleweke.
Kwanza, lugha ya Biblia iko wazi na inavutia. Badala ya kutumia maneno mengi yasiyoeleweka au magumu, Biblia hutumia maneno tunayoelewa. Mawazo magumu yanasimuliwa kwa maneno tunayotumia kila siku.
Kwa mfano, Yesu alifundisha mambo yaliyogusa mioyo ya watu kwa kuwasimulia mifano mingi rahisi iliyohusu mambo ya kawaida maishani. Baadhi ya mifano hiyo inapatikana katika Mahubiri ya Mlimani, yaliyoandikwa kwenye kitabu cha Biblia cha Mathayo, sura ya 5 hadi 7. Mchambuzi mmoja wa Biblia aliyeita mahubiri hayo “masomo yanayofaa,” alisema kwamba lengo lake “si kujaza habari nyingi akilini mwetu, bali kutuongoza na kutusaidia kutenda ifaavyo.” Huenda utatumia dakika 15 mpaka 20 ukisoma sura hizo, hata hivyo utashangaa jinsi maneno ya Yesu yalivyo rahisi kueleweka na yenye nguvu.
 Sababu nyingine inayofanya Biblia iwe rahisi kueleweka ni habari zilizo ndani yake. Si kitabu cha hekaya au mambo ya kubuniwa. Badala yake, kulingana na The World Book Encyclopedia kwa sehemu kubwa kitabu hicho kinazungumzia “kuhusu watu wakuu na wa kawaida” na pia “changamoto, matumaini, makosa, na mafanikio yao.” Ni rahisi kwetu kuelewa vizuri masimulizi hayo ya watu na matukio halisi na kujifunza masomo muhimu.—Waroma 15:4.

KINAPATIKANA KWA WOTE

Ni lazima kitabu kiwe katika lugha unayojua ili uweze kukielewa. Hata iwe unaishi wapi au unatoka taifa gani, huenda Biblia inapatikana katika lugha unayoelewa. Fikiria mambo yanayohusika ili jambo hilo liwezekane.

Utafsiri. Awali Biblia iliandikwa katika lugha ya Kiebrania, Kiaramu, na Kigiriki. Jambo hilo lilifanya watu wengi wasiojua lugha hizo washindwe kuisoma. Jitihada nyingi zimefanywa na watafsiri wanyoofu ili Biblia ipatikane katika lugha nyingi zaidi. Kwa sababu ya jitihada zao, leo Biblia imetafsiriwa ikiwa nzima au kwa sehemu katika lugha 2,700 hivi. Hilo linamaanisha kwamba zaidi ya asilimia 90 ya watu wanaweza kusoma sehemu fulani za Biblia katika lugha yao ya asili.

Uchapishaji. Awali, maandishi ya Biblia yaliandikwa katika vitu vinavyoweza kuharibika kama vile mafunjo na ngozi. Ili kufikisha ujumbe, maandishi hayo yalinakiliwa kwa uangalifu. Nakala hizo zilikuwa ghali sana na ni watu wachache tu walioweza kununua. Hata hivyo, baada ya uvumbuzi wa mashine ya kuchapa ya Gutenberg miaka 550 iliyopita, uchapishaji wa Biblia uliongezeka sana. Kulingana na ripoti moja, inakadiriwa kwamba nakala zaidi ya bilioni tano za Biblia, zikiwa nzima au kwa sehemu, zimegawanywa.
Hakuna kitabu chochote cha dini kinacholingana na Biblia. Kwa kweli, Biblia ni kitabu kinachoweza kueleweka. Hata hivyo, huenda isiwe rahisi kwako kuielewa. Lakini, unaweza kusaidiwa. Unaweza kupata wapi msaada huo? Utanufaikaje? Majibu yanapatikana katika makala inayofuata.


KAMA UNA MAONI YOYOTE NIANDIKIE HAPO CHINI AU TUMA UJUMBE KWENYE NO 0784 477775 au Whatup 0784 477775 AU FB Martin Malecela follow me in Twetter martmalecela au tembelea page yetu na ulike martmalecela.blogspot.com

Hakuna maoni: