Jumatano, 25 Februari 2015

KUUSHINDA ULIMWENGU – IV


“Basi, iwapo tunaye kuhani mkuu aliyeingia katika mbingu, Yesu, Mwana wa Mungu, na tuyashike sana maungamo yetu. Kwa kuwa hamna kuhani mkuu asiyeweza kuchukuana nasi katika mambo yetu ya udhaifu; bali yeye alijaribiwa sawasawa na sisi katika mambo yote, bila kufanya dhambi. Basi na tukikaribie kiti cha neema kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji(Waebrania 4:14-16).
Katika mfululizo wa somo hili la kuushinda ulimwengu, tumeweza kuona kanuni ya kuushinda ulimwengu, ambapo kuna mambo matatu (kuwa ndani ya Kristo, kuwa mtendaji wa Neno, na Kujilinda). Pamoja na mambo hayo, pia tumeona baadhi ya tabia za washindi ambazo ni (unyenyekevu na kumtegemea Mungu).
Katika somo hili, kuna mambo ya kujiuliza, Je! Katika ulimwengu tunashinda nini? Kuna mambo matano ya kuangalia hapa, kwenye Waebrania 4:14-16 kama ifuatavyo: mambo yetu ya udhaifu, majaribu, wakati wa mahitaji, na kutimiza wito wetu (yaani kwa mfano, Bwana Yesu alifanikiwa kutimiza wito wake kama kuhani mkuu na mpatanishi kati ya Mungu na mwanadamu).
Ukiyatazama mambo hayo matano, na kuyagawa katika mambo mawili makubwa, unaweza kusema kushinda dhambi na kutimiza wito wetu tulioitiwa. Shetani akishindwa kukuua (kwa maana yeye alikuwa muuji tangu mwanzo, na kazi yake ni kuiba, kuchinja na kuharibu), basi atakushawishi utende dhambi kwa kuitumia tamaa yako mwenyewe (mtu hujaribiwa na tamaa yake mwenyewe), na Ibilisi akishindwa hapo, basi atakupoteza kwenye malengo yako ili ushindwe kufanya mambo ya muhimu katika wito wako. Kama kuna janga kubwa ni kulima mashamba ya watu wakati lako limejaa nyasi; hivi ndivyo inavyokuwa kwa watu wengi ambao kwa kweli ni wachamungu sana, ila hawajui nafasi zao katika mwili wa Kristo, bali wao hufanya kilicho mbele yao au chenye maslahi ya dhahiri, kumbe! Hatukuitwa kufanya kitu chochote ila KILE Mungu alichotuitia kufanya. Huko nako ni kushindwa sana, yaani kushindwa kufanya mapenzi ya Mungu kwa wakati wake, hata kama hatutendi dhambi.
BWANA alijaribiwa katika mambo YOTE kama ilivyo sisi leo ila hakutenda dhambi (Waebrania 4:14-16) na kwa sababu hii basi, anaweza kutusaidia kwa habari ya “mambo yetu ya udhaifu” ambayo mengine ni magumu hata mchungaji wako akiyajua ataishia kukutenga tu. BWANA anaweza, ndio maana maandiko yamesema TUMTWIKE Yeye fadhaha zetu (1 Petro 5:7). Begani mwa Yesu kuna nafasi ya kutosha kubeba, sio shida zako tu ila na kukubeba wewe mwenyewe, kwa maana Yeye ni mchungaji na sisi ni kondoo; Mchungaji wa kondoo haoni shida kubeba kondoo begani mwake na kwenda kumtibu huko mbele. Kumbuka siku zote, ni wajibu wako KUJIWEKA mbali, au kujiepusha na DHAMBI IKUZINGAYO UPESI (Waebrania 12:1), na hii inatofautiana kati ya mtu na mtu, “ukijua mambo yako ya udhaifu”, imekupasa kuchukua hatua, japo kuna rehema na neema, ikibidi, kukimbia hata kwa jinsi ya mwili. Ndio maana BWANA alisema “jicho lako likikukosesha, aheri uling’oe na kulitupa” (Marko 9:47), hii inaonesha NAFASI yako katika USHINDI wako, na ndio maana ukisoma kitabu cha Ufunuo wa Yohana utaona majina ya watakaourithi Ufalme wa Mbinguni wanaitwa “washindi”, na huu ushindi waliupata DUNIANI yaani huku kwenye dhiki nyingi na mahitaji ya kila namna, ila walishinda.
Nafikiri imezoeleka sana kusikia watu wakisema “akipata shida, atarudi”, “akibwanwa, atalia”, “anajifanya mjanja kwa sababu anavyo, akiishiwa nitampata tu”, nk. Kama kuna mahali Ibilisi ameweka “nyavu” zake ni kwenye mahitaji yako. Anajua utakuja tu. Hii ni kanuni ya wavuvi wengi. Wavuvi hawakimbizi samaki, ila wanaweka “chambo”; samaki mwenye njaa (mhitaji) akija na njaa zake anakuwa mawindo mepesi! Ndio maana imekupasa kujua mitego hii, ukiona MAHITAJI yako (matumizi ya kawaida, cheo, pesa, chakula, kihisia, nk.) yanakufikisha mahali pa kutenda dhambi, jua hilo sio hitaji tena ila ni JARIBU! Jipange vyema, ukishinda utaitwa “mshindi”; lakini ukipata mahitaji yako na kuanguka, haikufai kitu hata kama ungepata ulimwengu wote kwa maana hapo umepoteza nafsi yako tayari.
Kumbuka siku zote, kuna rehema na neema, sawa, ila imekupasa kuchukua hatua za kukikariba Kiti cha neema, kwa ujasiri, ili tupewe rehema, na kupata neema ya kutusaidia wakati wa mahitaji  (Waebrania 4:16). Kweli Yesu anaweza kubeba mizigo yako, ila haji kuichukua ila wewe ndio “unamtwika” (1 Petro 5:7). Ukisubiri hapo chini, utaangamia kwa kukosa maarifa. Mungu anataka kuonekana kwako na kukuinua, ila imekupasa “KUMTAFUTA kwa BIDII” (Mithali 8:17; Yeremia 29:12-14) japo hayuko mbali nawe, ndipo utamwona!
Frank Philip.

KAMA UNA MAONI YOYOTE NIANDIKIE HAPO CHINI AU TUMA UJUMBE KWENYE NO 0784 477775 au Whatup 0784 477775 AU FB Martin Malecela follow me in Twetter martmalecela au tembelea page yetu na ulike martmalecela.blogspot.com

Hakuna maoni: